TFNC YAHIMIZA WANAOTOA USHAURI WA LISHE MITANDAONI KUSHIRIKIANA NA TAASISI ZENYE MAMLAKA


Na Mwandishi wetu Morogoro.

Taasisi ya Chakula na Lishe (TFNC) imewashauri  wataalam wa lishe na afya wanaotoa ushauri wa lishe kupitia mitandao ya kijamii kushirikiana na Taasisi zenye mamlaka ili kuhakikisha jamii inapata elimu sahihi yenye ushahidi wa kitaalamu.

Ofisa Lishe Na Mtafiti wa TFNC, Maria Ngilisho amesema hayo  katika Tamasha la Nne la Taifa la Utamaduni mkoani Morogoro na kuongeza kuwa  taasisi hiyo imepewa dhamana ya kuratibu shughuli za chakula na lishe, ikiwemo kufanya tafiti, kutoa elimu na kujenga uwezo kwa wadau mbalimbali.

Amesema ni kweli wapo wanaotoa huduma za lishe kwa jamii kupitia  mitandao ya kijamii na Taasisi  imekuwa ikiona hibyo inawahimiza kushirikiana nao ili kufikisha kile kinachotakiwa kwa jamii.


Amesema kaulimbiu ya taasisi hiyo katika tamasha hilo ni “Chakula Chetu, Utamaduni Wetu, Afya Yetu,” akisisitiza wananchi kula mlo kamili unaojumuisha vyakula kutoka katika makundi sita ili kupata virutubishi muhimu kwa afya.

Ngilisho amesema elimu hiyo inaambatana na umuhimu wa kuzingatia usafi wa mazingira, maji na chakula, kuepuka matumizi ya vileo, sigara na tumbaku, pamoja na kufanya mazoezi kwa angalau dakika 30 kila siku.

Kadhalika ameeleza kuwa maabara ya Taasisi ya Chakula na Lishe huchunguza sampuli za vyakula na binadamu ili kubaini virutubishi na upungufu wa vitamini au madini, huku matokeo yakitumika kutoa ushauri wa kitaalamu kwa Serikali kuhusu hatua za kukabiliana na changamoto za lishe.






Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MATOKEO YA UTAFITI WA HALI YA LISHE YA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI YATOLEWA

TFNC YAIBUKA MSHINDI WA JUMLA MAONESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI.

TUMIENI TAALUMA ZENU KUTATUA CHANGAMOTO ZA MASUALA YA CHAKULA NA LISHE KWENYE JAMII.