TUMIENI TAALUMA ZENU KUTATUA CHANGAMOTO ZA MASUALA YA CHAKULA NA LISHE KWENYE JAMII.

Na Mwandishi wetu-TFNC

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania Dkt. Germana Leyna, amefungua mafunzo elekezi kwa Waajiriwa wapya wa Taasisi, ambapo amewataka kutumia taaluma zao katika kusaidia kutatua changamoto mbalimbali za masuala ya chakula na Lishe zinazoikabili jamii.

Dkt. Germana amesema mafunzo hayo ya siku tano yamelenga kuwawezesha waajiriwa hao kujua mifumo mbalimbali ya kiutumishi, itakayowasaidia katika kutatua changamoto hizo, na kutekeleza majukumu mbalimbali ambayo Taasisi imekabidhiwa na Serikali kuyatekeleza.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania Dkt. Germana Leyna, akitoa maagizo  mbalimbali kwa waajiriwa wapya wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mafunzo elekezi   kuhusu sheria, kanuni na taratibu mbalimbali za utumishi wa umma.

“Mimi Matarajio yangu kwenu ni makubwa sana, mnisaidie kutatua changamoto za chakula na lishe kwa jamii na ndiyo changamoto ambazo sisi kama Taasisi ni jukumu ambalo tumekabidhiwa na serikali ili kuweza kulitekeleza.” amesema Dkt. Germana

Aidha Dkt. Germana amewataka waajiriwa hao kutokuwa sehemu ya walalamikaji kwa changamoto zilizopo ndani ya Taasisi bali wawe sehemu ya suluhisho ya changamoto hizo.

Waajiriwa wapya wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania, wakimsikiliza kwa makini Mkurugenzi wa Taasisi Dkt. Germana Leyna (hayupo pichani) wakati akifungua mafunzo elekezi kuhusu sheria, taratibu na kanuni za utumishi wa umma.

Kwa upande wake kaimu Mkurugenzi wa Fedha,Utumishi na Utawala Bw. Ally Said, amewataka  watumishi hao kuzingatia mafunzo wanayopatiwa kwani yatakuja kuwasaidia katika utekelezaji wa majukumu  mbalimbali ndani ya Taasisi.

Kaimu Mkurugenzi wa Fedha, Utumishi na Utawala Bw. Ally Said, wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania, akizungumza na waaajiriwa wapya wa Taasisi hiyo ( hawapo pichani) umuhimu wa kuzingatia mafunzo elekezi wanayopatiwa, ili kuwasaidia katika utekelezaji wa majukumu mbalimbali ndani ya Taasisi.

Kwa mujibu wa waraka namba 5 wa mwaka 2011 wa Utumishi, unaelekeza kila waajiriwa wapya ni lazima wapatiwe mafunzo elekezi ili kuwawezesha kufahamu uendeshaji wa shughuli mbalimbali za Taasisi husika, pamoja na kufahamu sheria mbalimbali za utumishi na utawala bora.

 

MWISHO:

 

 

 

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MATOKEO YA UTAFITI WA HALI YA LISHE YA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI YATOLEWA

TFNC YAIBUKA MSHINDI WA JUMLA MAONESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI.

WANAFUNZI WANYWE MAZIWA SHULENI-UMMY MWALIMU.