WADAU WA AFYA WAKUBALIANA KUANZISHA BENKI YA MAZIWA YA MAMA TANZANIA

Na, MwandishiWetu

Wadau wa Afya na Lishe nchini wamekutana na kufanya kikao kazi cha pamoja kujadili namna ya kuanzisha Benki ya Maziwa ya Mama, lengo likiwa kuboresha hali ya afya na lishe za watoto wachanga hususani wanaozaliwa na uzito pungufu, wagonjwa sana, ambao hawana mama au  mama zao ni wagonjwa mahututi na hivyo kukosa maziwa ya mama jambo linalosababisha athari kwa watoto kiafya na kuongeza vifo vya vichanga hivyo.

Akizungumza wakati wa kufungua kikao kazi hicho, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi kitengo cha Lishe Wizara ya Afya, Neema Joshua amesema kuwa Wizara ya Afya inaunga mkono jambo hilo na ipo tayari kushirikiana na wadau kuhakikisha linakamilika kwa wakati.

 “Niwapongeze wadau walioanzisha harakati hizi za kuanzisha Benki ya Maziwa ya Mama hapa Nchini kwa lengo la kuboresha hali ya afya na lishe za watoto wetu hususani wanaozaliwa na uzito pungufu au kabla ya wakati na mama zao kukosa maziwa ya kutosha jambo linalosababisha watoto hao kutokuwa vizuri” Amesema Neema Joshua.

Kwa upande wake Daktari wa Watoto kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila, Dkt. Lucy Mpayo amesema, Benki ya Maziwa ya mama ni huduma inayowawezesha akina mama kupata maziwa ya ziada, ambayo huchangiwa na wamama wengine kwa hiari na kuhifadhiwa kwa usalama kisha kupatiwa watoto wenye mahitaji. Uwepo wa benki ya maziwa  kutawezesha watoto hao kupata maziwa ya mama kwa muda muafaka na kusaidia kuimarisha afya zao, hususani kuongezeka uzito kwa haraka Zaidi.



Daktari wa Watoto kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili-Mloganzila, Dkt. Lucy Mpayo akiwasilisha mada wakati wa kikao cha wadau wa afya na lishe kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano hospitali ya Aga Khan, Dar es salaam.

Dkt. Lucy Mpayo aliendelea kuhimiza kuwa mtoto aliyezaliwa na uzito pungufu akiwahi kupewa maziwa ya mama katika siku za mwanzo baada za kuzaliwa humsaidia mtoto katika kumkinga dhidi ya maradhi na kumuwezesha kukua vizuri na hivyo kumpunguzia siku za kukaa hospitalini.

Aidha Dokta Lucy amesema kuwa Hosptali ya Taifa Muhimbili Mloganzila ilifanya utafiti wa mwaka mmoja kutoka Mei 2018 hadi Mei 2019 uliobaini kuwa asilimia 53 ya watoto waliozaliwa na uzito pungufu chini ya kilo moja na nusu huchelewa kuanzishiwa kupewa maziwa ya mama kwa zaidi ya siku mbili kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo mama kuwa mgonjwa baada ya kujifungua, kutokuwa na maziwa ya kutosha pamoja na mtoto kuwa mgonjwa.


Daktari wa Watoto kutoka PATH-Nairobi Kenya, Dkt. Emily Njuguna akitoa uzoefu kwa njia ya mtandao juu ya uanzishwaji wa benki ya maziwa ya mama kwa washiriki wa kikao kazi cha wadau wa afya na lishe kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano hospitali ya Aga Khan, Dar es salaam.

Uanzishwaji wa Benki ya Maziwa ya Mama ulianza rasmi mwaka 1909 nchini Austria na kufuatiwa na Amerika ya Kaskazini mwaka 1919 na kisha kuenea katika nchini nyingine. Mwaka 1980 Benki nyingi za Maziwa ya Mama zilifungwa kutokana na hofu ya maambukizi ya Virusi vya Ukimwi, lakini baada ya mikakati mingi kuanzishwa ya kuzuia maambukizi ya vijidudu vya Virusi kwa kuwafanyia vipimo akina mama wanaochangia maziwa yao na kisha kuyahifadhi maziwa hayo kwa usalama zaidi benki hizo zilifungiliwa tena. Benki ya kwanza ya maziwa  kuanzishwa Afrika ilikuwa Afrika Kusini iliyoanzishwa mwaka 1980, na kisha kufuatiwa na Cape Verde 2011. Kwa upande wa nchi za Afika Mashariki Kenya ndio nchi ya kwanza kuanzisha Benki ya Maziwa ya Mama  mwaka 2019.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MATOKEO YA UTAFITI WA HALI YA LISHE YA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI YATOLEWA

TFNC YAIBUKA MSHINDI WA JUMLA MAONESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI.

WANAFUNZI WANYWE MAZIWA SHULENI-UMMY MWALIMU.