BUNDA WAZINDUA KAMPENI YA MWEZI WA AFYA NA LISHE YA MTOTO
Mkuu wa Wilaya ya Bunda Dkt. Vicent Naano amezindua kampeni ya Mwezi wa Afya na Lishe ya Mtoto katika halamshauri hiyo, ambap amewataka wazazi na walezi kuhakikisha wanawapeleka watoto wao wenye umri wa miezi 6 hadi 59 kupatiwa matone ya Vitamini A na dawa za kuzuia maambukizi ya Minyoo.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa zoezi hilo, Dkt
Naano ameserma uongozi wa awamu ya sita chini ya Rais Mhe. Dkt Samia Suluhu
Hassan, unatoa kipaumbele katika masuala ya lishe kwa kuboresha huduma za afya
na lishe, ikiwemo utoaji wa matone ya Vitamini A, na dawa za kuzuia maambukizi
ya Minyoo ambazo hutolewa bila malipo.
Dkt. Naano amesema kampeni ya Afya na Lishe ya Mtoto ni muhimu katika kutokomeza matatizo yatokanayo na upungufu wa vitamini na madini kwa watoto wetu na husaidia katika kuimarisha afya na lishe zao na kuleta tija katika taifa pindi wanapokuwa watu wazima.
“Hili suala la lishe ndugu zangu ni suala muhimu sana
na Mama Samia analisisitiza sana, ili kuhakikisha kwamba taifa letu linakuwa na
watoto wanaokuwa vizuri kimwili na kiakili” Takwimu zinaonesha kuwa watoto 836 katika
halmashauri yetu hawakufikiwa wakati wa utekelezaji wa kampeni hii. Watoto hawa
ni wengi sana. Hivyo nitoe wito kwa wazazi na walezi kuhakikisha tunapeleka
watoto wetu katika vituo vya kutolea huduma za afya ili wapatiwe huduma hizi”
Amesema Dkt. Naano.
Kampeni ya Mwezi wa Afya na Lishe ya Mtoto ni kampeni ya kitaifa inayotekelezwa nchi nzima mara mbili kwa mwaka (tarehe 1 hadi 30 ya mwezi Juni na 1 hadi 31 ya mwezi Disemba). Kampeni hii hufanyika kwa watoto wenye umri wa miezi 6 hadi 59 kupatiwa matone ya Vitamini A na dawa za minyoo zinazotolewa bila malipo katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa lengo la kuimarisha hali za lishe na kutokomeza udumavu kwa watoto
Maoni
Chapisha Maoni