TFNC YATOA MAFUNZO KWA WAUGUZI NA WAKUNGA

Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania imeendesha kozi fupi kwa wauguzi na wakunga, juu ya kumsaidia mama kunyonyesha kwa usahihi kwa lengo la kuwajengea uwezo zaidi na kufanikisha utoaji wa huduma bora zitakazosaidia kutokomeza utapiamlo kwa watoto.

 

Akizungumza  wakati wa kugawa vyeti kwa wahitimu wa kozi hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe Tanzania, Dkt. Germana Leyna  amesema,  mafunzo hayo yatawasaidia wahitimu kuongeza ufanisi katika maeneo yao ya kazi na kutoa huduma bora kwa wanawake wanaojifungua na kunyonyesha jambo litakalosaidia kwa kiasi kikubwa kuboresha hali ya lishe za watoto  wa kitanzania.



“Mafunzo haya yametolewa kwa njia ya majadiliano kati ya washiriki na wawezeshaji, jambo litakalosaidia Taasisi kubaini changamoto zinazowakabili kina mama kushindwa kunyonyesha ipasavyo na hivyo kuwafundisha wauguzi na wakunga namna bora za kutatua changamoto hizo na hatimaye kumwezesha mama kunyonyesha kwa usahihi” Amesema Dkt. Leyna.


Aidha Dkt. Leyna amewaomba wahitimu wa kozi hiyo kuwa mabalozi wazuri kwa kuboresha utendaji wao wa kazi na kuwahamasisha wengine kuja kusoma kozi hiyo pindi itakapotangazwa tena.

Awali wakati akimkaribisha Mkurugenzi Mtendaji kufunga mafunzo hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Elimu na Mafunzo ya Lishe, Dkt. Esther Nkuba amesema kuwa wauguzi na wakunga ni watu muhimu sana katika kufanikisha suala la unyonyeshaji katika jamii.

 

“Takwimu za mwaka 2022 za TDHS zinatuonesha kuwa watoto wanaoanzishiwa kunyonyesha maziwa ya mama ndani ya saa moja ni baada ya kuzaliwa ni asilimia 70, na watoto wanaopewa maziwa ya mama pekee katika miezi sita ya mwanzo ni asilimia 64, lengo letu ni kufika asilimia 100, na hili linawezekana ndio maana tumeanza kutoa mafunzo haya kwa wauguzi na wakunga kwa sababu ni watu muhimu sana katika kufanikisha unyonyeshaji katika jamii” Amesema Dkt. Nkuba.

 

Kwa upande wake Mratibu wa Mafunzo hayo Eliasaph Mwana amesema kuwa kozi hii imetolewa kwa siku nne kuanzia tarehe 23/05/2023 hadi tarehe 26/05/2023 ambapo jumla ya watu watano waliweza kushiriki na kuhitimu mafunzo hayo.



“Jumla ya watu 30 walifanya maombi ya kusoma kozi hii lakini walioweza kujiunga na kuhudhuria ni watu watano tu, hivyo tutafanya tathimini kubaini ni changamoto gani zilizosababisha wau wengi kushidwa kuhudhuria ili tutakapotangaza tena kozi hii watu wengi waweze kuhudhuria” amesema Mwana.

 

Naye Mkunga kutoa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi, Anitha Mganga ambeaye amehudhuria mafunzo hayo ametoa rai kwa TFNC kuangalia ni kwa namna gani wataweza kutoa mafunzo haya mikoani ili kuhakikisha elimu hii inawafikia watu wengi zaidi.

 

 


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MATOKEO YA UTAFITI WA HALI YA LISHE YA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI YATOLEWA

TFNC YAIBUKA MSHINDI WA JUMLA MAONESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI.

WANAFUNZI WANYWE MAZIWA SHULENI-UMMY MWALIMU.