UMMY MWALIMU: TUTANDELEA KUTOA AJIRA KWA WAUGUZI NCHINI

UMMY MWALIMU: TUTANDELEA KUTOA AJIRA KWA WAUGUZI NCHINI

Na, WAMJW                       

Serikali imesema itaendelea kutoa kipaumbele katika ajira za wauguzi kadri nafasi zitakavyokuwa zikipatikana ili kuboresha huduma za afya nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo  na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati akizungumza na watumishi wa hospitali ya rufaa ya mkoa ya Mwananyamala katika Maadhimisho ya Siku ya Waguzi Duniani  ambayo huadhimishwa tarehe 12 Mei kila mwaka. Kauli mbiu ya mwaka huu ni “Wauguzi; Sauti inayoongoza Uuguzi kwa Dunia yenye Afya.”

Waziri Ummy Mwalimu amesema Serikali itaendelea kutoa kipaumbele katika ajira za wauguzi kwa sababu kuna uhaba wa wauguzi kwenye vituo vya afya licha ya kuwapo zaidi ya wauguzi 30,451 katika vituo vya umma na binafsi nchini.

Amesema asilimia 80 ya huduma  za afya katika vituo vya kutoa huduma za afya zinatolewa na wauguzi hivyo Serikali itaendelea kutambua na kuthamini kazi nzuri zinazofanywa na wauguzi nchini.

 “Wauguzi wamekuwa wapambanaji wakubwa katika kutoa huduma kwa washukiwa wa ugonjwa wa Corona (Covid-19), hivyo hongereni  wauguzi wote nchini Tanzania,” amesema Waziri.

Amesema katika jitihada za Serikali za kuboresha huduma za wauguzi na wakunga, Serikali imekamilisha muongozo wa kutoa huduma kwa kuzingatia utu, heshima na maadili.

 

Waziri wa Afya amesema jumla ya waguzi 778 katika hospitali 15 za rufaa za mkoa wamepatiwa mafunzo muhimu ili kuwezesha mpango wa kutoa huduma rafiki kwa wananchi na kwa kujali utu wao.

“Mafunzo haya yataendelea kutolewa katika ngazi zote za kutoa huduma na tayari tumetengeneza mfumo wa kupokea taarifa za malalamiko na kero kutoka kwenye vituo vya kutolea huduma,” amesema Waziri Ummy Mwalimu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu, akisikiliza maelezo kutoka kwa  kaimu Mganga mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mwanyamala Dkt: Isdory Kiwale baada ya kufanya ziara hospitalini hapo, kuangalia utoaji wa huduma za afya, kushoto kwake ni Rais wa Chama cha Wauguzi na Wakunga Tanzania (TANNA) .

Naye Rais wa Chama cha Wauguzi na Wakunga Tanzania (TANNA), Bw. Alexander Baluhya amesema ili kuwapo kwa huduma bora na salama za afya, nchi inapaswa kuwa na wataalamu wenye weledi wa hali ya juu na mazingira bora ya kazi.

“Hivi sasa nchi yetu ina wauguzi 30,451 waliojiriwa katika sekta ya afya ambao ni takribani asilimia 60 ya wataalamu wote wa afya. Wauguzi hawa wanatoa zaidi ya asilimia 80 ya huduma za afya ambazo zimekuwa zikitolewa kwa Watanzania. Hivyo upungufu wa wauguzi na wakunga ni  asilimia 48,” amesema Bw. Baluhya.

Bw. Baluhya amewapongeza wauguzi  nchini kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia maadili ya taaluma yao hasa katika kipindi hiki cha maambukizi ya virusi vya Corona (Covid-19).


Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

MATOKEO YA UTAFITI WA HALI YA LISHE YA WANAFUNZI SHULE YA MSINGI YATOLEWA

TFNC YAIBUKA MSHINDI WA JUMLA MAONESHO YA SIKU YA CHAKULA DUNIANI.

WANAFUNZI WANYWE MAZIWA SHULENI-UMMY MWALIMU.